Monday, January 21, 2013

JE,HUU NI UBINADAMU???


Na;Dovakmwene John Mscheshi


Kifo ni kitu kinachoweza kumtokea mtu yoyote na wakati wowote kwani tunaamini ni mipango ya Mungu. Kifo hutokea katika mazingira tofauti ikiwa ni pamoja na maradhi, ajali mbalimbali, vita/mapigano, ugomvi na kadhalika.
Vifo vipo vya ghafla pasipo kutarajia, vingine vikitokana na kuugua muda mfupi au mrefu. Mtu anapofariki shughuli za mazishi huandaliwa ambapo waombolezaji hukusanyika nyumbani kwa marehemu au sehemu iliyopangwa na wanafamilia kwa msiba.
Pale kwenye maombolezo huwa na pilikapilika nyingi huku ratiba ya maandalizi ikitangazwa kila inapobidi. Waombolezaji huonekana katika makundi wakiteta huku wengine wakiwa wamejawa na simanzi.
Pamoja na ukweli huo, tabia hizi hazipendezi. Kwa mfano, lipo jambo moja au niseme tabia ambayo imezoeleka kwa waombolezaji wengi kuonekana wakijadili zaidi chanzo cha kifo cha marehemu badala ya kutafakari hatma yao waliobaki duniani na kumuombea aliyetangulia mbele za haki.
Kwa maneno mengine, wapo watu wanaogeuza msiba kama vijiwe vya kumjadili marehemu. Na watu hawa, hata wakati wa uhai wake hawakuwa kusema juu yake hadharani penye kadamnasi ya watu, lakini leo kafariki wanazusha hata yale yaliyofichika. Hebu tujiulize, hivi yanahusu? Na kwanini wanadamu tuko hivi? Hii ni kasoro kubwa sana yafaa tubadilike.
Utasikia fulani wakati wa uhai wake alikuwa anaringa sana. Ebo! Ulitaka afanyeje. Hivi hujui maringo ni afya na kinyume chake ni kasoro? Kuringa ni kujisikia furaha kwa uhai wako. Ndio, usibishe.
Mara utasikia fulani alikuwa kiruka njia, alipenda sana wanaume au wanawake, alipenda sana wake au waume za watu…Oh, ameacha watoto wa baba tofauti, amekufa na gonjwa baya, eti angezingatia ushauri wa daktari yasingemsibu hayo, ili mradi ni maneno ya hovyo, kisa anayezungumzwa ameshajifumzikia.
Wengine utasikia eti laana ya baba au mama yake ndio imemuua. Ili mradi mtu atoe neno kinywani mwake kufurahisha jopo pale kwenye maombolezo. Hili siyo jambo zuri hata kidogo, hasa ikizingatiwa kuwa kila mtu anayo mapungufu yake na hakuna atakayeishi milele nikiamini kile alichowahi kuniambia bibi yangu kuwa “Uyana nyi maseiyano” yaani “Dunia ni mapishano”.
Tabia nyingine inayokera wakati wa msiba ambayo wengi bado wanaiendekeza ni kule baadhi ya ndugu kugombea mali za marehemu zikiwemo nguo zake. Eti kufa kufaana na kwamba aliyekufa kafa hivyo mali zake ni halali kwa wengine. Lo! Makubwa kwani madogo yana unafuu.
Nimewahi kushuhudia ndugu wakichukua nguo za marehemu kwa kuzificha na kuondoka nazo, tena mwili wa marehemu ukiwa bado chumba cha maiti hospitalini. Yaani mwili haujazikwa, tayari watu wanajigawia mali zake. Ni tabia mbaya sana hii. Wenye tabia hii wasidhani ni kirahisi hivyo, yapo madhara yake. Kwanini mtu asisubiri kupewa mali chini ya taratibu za kifamilia?
Lingine ambalo halina sura nzuri walifanyalo wanadamu ni kule kukimbilia kuuona mwili wa marehemu wakati hapa alipokuwa mgonjwa hakuwahi kwenda kumjulia hali achilia mbali kumsaidia fedha za matibabu. Hukimbilia kuona kafa na afya yake au kakonda? Acheni jamani, mzaha huu, ni dhambi.
Mpenzi msomaji, hebu niulize; lipi ni jema katika haya mawili:- kumtembelea mgonjwa na ikibidi kumsaidia fedha za matibabu au kule kwenda mchanga rambirambi baada ya kufa?
Wapo wale ambao hawakujua fulani alikuwa mgonjwa, lakini wakasikia amefariki. Lakini wengine, pengine mahasimu waliowahi kukwaruzana, wakisia fulani kafa huachia; “acha afe”. Yaani hawaoni kwamba hiyo ni njia yao pia. Huu siyo ubinadamu. Maisha ya mtu yanapotoweka lazima usikitike kwani hutamuona tena katika maisha haya ya kidunia. Na utambue nawe kifo kinakusubiri.
Nakumbuka bibi mzaa mamangu wakati wa uhai wake kila nilipomtembelea alikuwa anafurahi sana pale ninapompelekea zawadi ambapo husema; “Afadhali uniletee watati ningali hai, kwani nikishafumba macho(kufa) utakachoniletea ni bure”. Yalikuwa ni maneno yaliyobeba ujumbe mzito sana.
Ndio maana ni muhimu sana hata pale mwenzako anapokuwa mgonjwa yafaa tumhudumie kwa nguvu zote, tumsaidie chakula, dawa badala ya kusubiri azimike ndipo tupige mikono mifukoni kutoa rambirambi.
Sisemi watu wasitoe rambirambi, la hasha. Ninachosema hapa ni kwamba tutizame mazingira yenyewe, kama ni kifo cha ghafla ni sawa. Lakini kama ni kifo kinachotokana na maradhi tusaidiane wakati wa uhai badala ya kubezana. Pengine msaada wako unaweza kumsogezea mgonjwa maisha akakamilisha mipango yake duniani au hata akapona kabisa. Maisha Ndivyo Yalivyo.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI     

No comments:

Post a Comment